MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu,
imewahukumu kwenda jela miaka 55 mume na mkewe, baada ya
kupatikana na hatia ya
kuratibu na kuuza nyara za serikali, yakiwamo meno na mifupa ya tembo kilo
450.6 yenye thamani ya Sh. bilioni 2.2.
Washtakiwa hao Peter Kabi (45) na mkewe, Leonidia Kabi
(46), walikutwa na nyara hizo sawa na tembo 93 waliouawa, wakiwa wamezihifadhi
kwenye jeneza na kufunikwa na bendera ya taifa.
Mahakama hiyo chini ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi,
pia iliamuru nyara walizokutwa nazo washtakiwa zitaifishwe na serikali.
Hakimu Shaidi alisema ushahidi wa mtaalamu wa
wanyamapori, Emmanuel Lyimo, ulibainisha kuwa miongoni mwa hasara zinazotokana
na kuuawa tembo ni uchumi kushuka.
“Washtakiwa wamekutwa na nyara hizo ambazo ni sawa na
tembo 93 waliouawa ... kwa maana hiyo itachukua muda mrefu tembo 93 kuzaliwa,”
alisema Hakimu Shaidi na kuongeza:
“Ninyi washtakiwa mmeamua kula matunda ya taifa hili kinyume
cha utaratibu ... siyo sahihi mjinufaishe mke na mume, mnastahili kutumikia
kifungo cha miaka 15 (kwa) kosa la kwanza, miaka 20 kosa la pili na 20 mingine
kwa kosa la tatu na adhabu yote itakwenda sambamba.”
Akizungumzia ombi la Jamhuri kuhusu kutaifishwa nyumba
iliyokuwa imehifadhi nyara hizo, Hakimu alisema upande wa Jamhuri uwasilishe
maombi yenye vielelezo vya kuthibitisha umiliki halali wa washtakiwa ili
mahakama yake itoe uamuzi.
Kabla ya hukumu hiyo, upande wa Jamhuri ukiongozwa na
Mawakili wa Serikali, Paulo Kadushi na Elias Athanas uliomba mahakama
ijielekeze katika kifungu cha 111 cha Sheria za Wanyamapori kinachotoa masharti
ya lazima.
Kadushi alidai kifungu hicho kinaeleza kwamba mtuhumiwa
akikutwa na hatia nyara na kitu chochote kilichotumika kuhusiana na nyara hizo,
vyote vinataifishwa.
“Mheshimiwa, naiomba mahakama yako ijielekeze kwenye
kifungu hicho kwa kutaifisha meno na mifupa ya tembo waliyokutwa nayo
washtakiwa na nyumba iliyokuwa imehifadhi nyara hizo kwa kuwa inamilikiwa na
washtakiwa wote wawili,” alidai Kadushi.
Upande wa utetezi ulipopewa nafasi ya kuomba kupunguziwa
adhabu, ulidai kuwa washtakiwa ni mke na mume ambao wana watoto wawili, wazazi
na ndugu wanaowategemea, hivyo uliomba mahakama kuwapunguzia adhabu na
kutoitaifisha nyumba wanayoimiliki.
Hakimu alisema kwa kuwa washtakiwa walijipendelea kula
keki ya taifa kinyume cha taratibu, watakwenda jela kutumikia kifungo hicho na
haki ya rufani kwa upande ambao haujaridhika iko wazi.
AIBU KUBWA
Baada ya kutolewa hukumu hiyo, Mkurugenzi wa Wanyamapori, Alexandra Sogorwa, aliwaambia waandishi wa habari katika viunga vya mahakama hiyo kuwa ni aibu kubwa Tanzania kutoka kuwa na tembo zaidi ya 100,000 miaka 10 iliyopita hadi kufikia 50,000.
Baada ya kutolewa hukumu hiyo, Mkurugenzi wa Wanyamapori, Alexandra Sogorwa, aliwaambia waandishi wa habari katika viunga vya mahakama hiyo kuwa ni aibu kubwa Tanzania kutoka kuwa na tembo zaidi ya 100,000 miaka 10 iliyopita hadi kufikia 50,000.
“Tusaidiane kupambana kutokomeza ujangili dhidi ya
wanyama wetu, wakiwamo tembo," alisema kwa sababu "hali ni mbaya na
ni aibu kubwa Mtanzania kuanza kupanda ndege kwenda kuangalia tembo nchini
Marekani.”
“Rais ametupa majukumu kupambana na ujangili kiasi kwamba
jangili akimuona tembo akimbie ... mahakama imetoa haki kwa pande zote mbili
katika kesi hii.”
Naye Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Biswalo Mganga
aliyekuwa katika mkutano huo na waandishi wa habari alisema:
"Familia moja inahujumu uchumi wa taifa, wamekutwa
na nyara za Sh. bilioni 2.2, kwa kweli hii haiwezi kuvumilika, tusaidiane
kutokomeza wahujumu uchumi.
“Washtakiwa walitumia mbinu ya kuweka meno ya tembo
kwenye jeneza na kufunika na bendera ya taifa letu wakijifanya wanasafirisha
maiti ya askari polisi, kwa kweli hii ni hatari.
"Tusaidiane wanahabari muwaeleze wananchi hasara
tunayopata ni yetu sote.”
Biswalo alisema familia moja imeangamiza tembo 93 na
kwamba huo ni uhujumu wa hali ya juu.
Katika kesi ya msingi, washtakiwa walidaiwa kuwa Oktoba
27, 2012 katika sehemu tofauti kati ya Dar es Salaam na Iringa, waliratibu
kufanyika kwa makosa ya kukusanya na kuuza nyara hizo.
Katika shtaka la pili, ilidaiwa kuwa siku ya tukio la
kwanza, eneo la Kimara Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, walikutwa na
meno 210 yenye uzito wa kilo 450.6 yakiwa na thamani ya Sh. bilioni 2.1 sawa na
tembo 91.
Katika shtaka la tatu, ilidaiwa kuwa siku ya tukio la
kwanza, walikutwa na mifupa mitano ya tembo ikiwa na thamani ya Sh. milioni
47.4 sawa na tembo wawili.
NA:
Hellen Mwango

Comments
Post a Comment